

Serikali imetoa rai kwa wadau wa mashirika yasiyo ya kiserikali kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuimarisha mahusiano ya kikazi kati ya Serikali na wadau hao, pamoja na kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Rai hiyo ilitolewa na Kaimu Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Wizara ya Fedha, Bw. John Kuchaka, wakati akifungua warsha ya siku moja iliyokutanisha washiriki wa mashirika yasiyo ya kiserikali Tanzania Bara kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Lindi, Mwanza, Pwani, Mtwara, Kagera na Arusha, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano. Warsha hiyo ilifanyika katika ukumbi wa Ofisi za Bunge, jijini Dar es Salaam.
Alisema warsha hiyo itawezesha washiriki kuelewa kuhusu ushirikiano kati ya Serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali hapa nchini ili kuimarisha ufanisi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya kijamii.
‘‘Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha kuwa maendeleo ya wananchi yanapatikana kwa njia jumuishi na endelevu, hivyo mchango wa mashirika yasiyo ya kiserikali ni muhimu sana, hasa katika kufikisha huduma kwa jamii na kuunga mkono juhudi za Serikali katika sekta mbalimbali,’’ alisema Bw. Kuchaka.
Bw. Kuchaka alisema kuwa ni muhimu kuwa na uelewa wa pamoja kuhusu mifumo, taratibu na miongozo inayosimamia utekelezaji wa shughuli za maendeleo ili kuwezesha ushirikiano huo uwe na tija na kufikia malengo.
‘‘Wadau wote ni muhimu kuelewa miongozo muhimu, ikiwemo Mwongozo wa Uzingatiaji wa Fedha na Ushirikiano na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Mwongozo wa Bajeti ya Serikali pamoja na Miongozo ya Uratibu na Ushirikiano wa Maendeleo. Hivyo, kupitia warsha hii tunatarajia sote kujenga uelewa wa pamoja,’’ alisema Bw. Kuchaka.
Alisisitiza washiriki wa warsha hiyo kutumia fursa ya mafunzo kubaini maeneo yanayohitaji maboresho ili kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.
Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa warsha hiyo, Katibu Mkuu wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Bi. Fransisca Mboya, alisema kupitia warsha hiyo wamejifunza namna bora ya kuwasilisha shughuli na mchango wa mashirika yao ili yatambulike zaidi kitaifa kwa kazi wanayofanya, hususan katika utekelezaji wa miradi mbalimbali na utoaji wa huduma kwa jamii.
‘‘Tumefurahia majadiliano na mada zilizowasilishwa, na mwisho tumetoa mapendekezo yetu ya namna bora ya kuboresha mahusiano kati ya mashirika yasiyo ya kiserikali na Serikali,’’ alisema Bi. Mboya.
Aidha, walitoa rai kuwa mafunzo kama hayo yawe endelevu ili kuendelea kuwajengea uwezo wadau wote, hasa katika masuala ya usimamizi wa fedha, hatua itakayohakikisha kuwa kuna ushirikiano imara na endelevu katika kuleta mabadiliko chanya ya kijamii na kiuchumi.






