Na Neema Kandoro Mwanza
WIZARA ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imetatua migogoro 945 na kutoa hati zaidi ya 1000 katika Halmashauri za wilaya nne Mkoani Mwanza kwa kipindi cha Mwezi Oktoba hadi Disemba huku zoezi likiendelea kufanyika ngazi za kata.
Hayo yamebainishwa leo Jijini Mwanza na Kamishina Msaidizi Mkoani hapa Happiness Mtutwa akisema kuwa wilaya ya Ilemela migogoro 243 ilitatuliwa huku Nyamagana migogoro 570 ilipata ufumbuzi huku utoaji wa Elimu ukipewa nafasi kwenye matukio hayo.
Aliendelea kusema kuwa katika wilaya ya Misungwi migogoro 106 ilipata ufumbuzi na Magu migogoro 26 imetatuliwa huku zoezi hilo likiendelea kufanyika kwenye eneo hilo.
Mtutwa alisema kutokana na hitaji la Serikali kuwataka kuwasogelea karibu wananchi Ili kuwatatulia wananchi kero zao wameanzisha Kliniki ya Ardhi ambayo imepata ufanisi katika maeneo waliyopita.
Alisema kuwa mwakani wanakusudia kutoa elimu kwa muda mrefu kwa watu wengi kwenye maeneo ambayo yatawezesha watu wengi kufika na yatajumuisha viongozi mbalimbali wa serikali Ili kumaliza kero za ardhi kwa wananchi.








