Home Kitaifa TANZANIA YAPATA SH. BILIONI 60.7 KUBORESHA HUDUMA ZA MAJI

TANZANIA YAPATA SH. BILIONI 60.7 KUBORESHA HUDUMA ZA MAJI

Na.Alex Sonna-DODOMA

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesaini mkataba wa msaada wenye thamani ya Euro milioni 20, sawa na Shilingi bilioni 60.7, kutoka Serikali ya Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW),kwa ajili ya kutekeleza mradi mkubwa wa kuboresha huduma za usambazaji maji, usafi wa mazingira na usimamizi wa rasilimali za maji katika miji ya Tunduma na Vwawa-Mlowo mkoani Songwe.

Hatua hiyo inayotajwa kuwa sehemu ya juhudi za kuimarisha huduma za kijamii na kukuza maendeleo endelevu katika maeneo yenye mahitaji makubwa ya miundombinu ya maji.

Akizungumza leo Juni 22,2026 jijini Dodoma baada ya kusaini mkataba huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, amesema  mradi huo utaleta mageuzi makubwa katika sekta ya maji kwa kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama, kuboresha usafi wa mazingira na kuimarisha afya za wananchi.

Ameeleza kuwa fedha hizo zitatumika kujenga na kuboresha miundombinu ya usambazaji wa maji, kuongeza miunganisho ya wateja, kujenga mtambo wa kisasa wa kutibu majitaka, kununua magari ya kunyonya majitaka pamoja na kujenga miundombinu ya usafi wa mazingira katika taasisi mbalimbali za umma ikiwemo shule shule zilizochaguliwa.

“Mradi huu utaongeza upatikanaji wa huduma bora za maji na usafi wa mazingira kwa maelfu ya wananchi wa Tunduma na Vwawa-Mlowo, huku ukiimarisha usimamizi wa rasilimali za maji na kuchangia ustawi wa jamii kwa ujumla,” amesema Dkt. Mwamba.

Amesema uwekezaji huo ni sehemu ya ushirikiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Ujerumani ambao umeendelea kuzaa matunda katika sekta mbalimbali muhimu za maendeleo.

Dkt. Mwamba ameipongeza Serikali ya Ujerumani kwa kuendelea kuiunga mkono Tanzania katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, akibainisha kuwa misaada inayotolewa imechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini kupitia sekta za maji, afya, uhifadhi wa mazingira, usimamizi wa fedha za umma na usawa wa kijinsia

Aidha, amesisitiza  kuwa katika mazungumzo ya maendeleo kati ya Tanzania na Ujerumani yaliyofanyika Dar es Salaam Machi 2024, Serikali ya Ujerumani iliahidi kutoa msaada wa Euro milioni 70 kwa ajili ya kufadhili miradi mbalimbali ya maendeleo nchini, jambo linalodhihirisha kuimarika kwa ushirikiano wa kihistoria kati ya mataifa hayo mawili.

Dkt. Mwamba,amesema mradi huo unaendana na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Mpango wa Tatu na wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano unaolenga kukuza uchumi shindani na kuboresha maisha ya wananchi.

Amesisitiza kuwa Serikali chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, itaendelea kuimarisha ushirikiano wa maendeleo na washirika wa kimataifa huku ikihakikisha miradi yote inayofadhiliwa inatekelezwa kwa ufanisi ili wananchi wanufaike na matokeo yaliyokusudiwa.

Kwa upande wake Naibu Balozi wa Ujerumani nchini, Manuel Muller, amesema Tanzania na Ujerumani zimeendelea kuwa washirika wa maendeleo kwa zaidi ya miaka 60, huku sekta ya maji ikiwa miongoni mwa maeneo yaliyotoa matokeo makubwa kwa maisha ya wananchi.

Amesema kupitia ushirikiano huo, zaidi ya wananchi 500,000 katika mikoa ya Kigoma, Lindi na Sumbawanga wamepata huduma za uhakika za maji safi na usafi wa mazingira kupitia miradi mbalimbali iliyofadhiliwa na Serikali ya Ujerumani.

“Tanzania ni miongoni mwa washirika wakubwa wa Ujerumani katika ushirikiano wa kifedha. Kwa sasa tunatekeleza miradi yenye thamani ya zaidi ya Euro milioni 400. Maji na usafi wa mazingira ni haki ya msingi ya binadamu, na tutaendelea kushirikiana kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata huduma hizo muhimu,” amesema  Muller.

 Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) nchini Tanzania, Vanessa Eidt, amesema mradi huo una umuhimu mkubwa kwa kuwa unagusa moja kwa moja maisha ya wananchi, akibainisha kuwa upatikanaji wa maji safi ni msingi wa maendeleo ya uchumi, afya bora na usalama wa chakula.

Amesema Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imeweka kipaumbele katika uhifadhi wa mazingira na usimamizi endelevu wa rasilimali za maji, hivyo KfW itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kufanikisha malengo hayo ya maendeleo.

Naye  Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Mwajuma Waziri,amesema mradi huo umefika wakati muafaka kutokana na athari zinazoongezeka za mabadiliko ya tabianchi pamoja na kasi ya ukuaji wa miji inayoongeza mahitaji ya huduma za maji.

Amesema utekelezaji wa mradi huo utaimarisha usimamizi wa rasilimali za maji unaozingatia mabadiliko ya tabianchi na kuongeza upatikanaji wa huduma za maji salama kwa wananchi wa Tunduma na Mlowo.

Mhandisi Mwajuma amebainisha kuwa Tanzania imeendelea kunufaika na ushirikiano wa muda mrefu na Serikali ya Ujerumani pamoja na KfW, ambapo miradi kadhaa ya maji imekamilika na kuboresha maisha ya wananchi katika maeneo mbalimbali ya nchi, ikiwemo Programu ya Seven Towns iliyotekelezwa katika mikoa ya Kigoma, Lindi na Sumbawanga.

Ameongeza kuwa ushirikiano huo unaendelea pia katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati, ikiwemo Mradi wa Maji wa Simiyu, huku mradi wa Tunduma na Mlowo ukiwa sehemu ya juhudi za Serikali za kuhakikisha usalama wa maji na ustawi wa wananchi vinaimarika zaidi.

“Wizara ya Maji itaendelea kusimamia utekelezaji wa mradi huu kwa uwazi, ufanisi na kwa wakati, kwa kushirikiana na wadau wote, ili manufaa yake yawe ya kudumu kwa wananchi na kuchangia kufikiwa kwa Malengo ya Maendeleo Endelevu, hususan lengo la sita linalohusu maji safi na huduma bora za usafi wa mazingira,” amesema Mhandisi Mwajuma.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here
Captcha verification failed!
CAPTCHA user score failed. Please contact us!