Home Burudani TAMRISO YATANGAZA TENDA KWA MAWAKALA KUKUSANYA MAPATO YA KAZI ZA MUZIKI

TAMRISO YATANGAZA TENDA KWA MAWAKALA KUKUSANYA MAPATO YA KAZI ZA MUZIKI

KAMPUNI ya kuuza leseni ya matumizi ya muziki na kugawa mirabaha (Tamriso) imetangaza tenda kwa mawakala kuomba kibali kwa ajili ya kupata leseni ya kukusanya mapato yatokanayo na biashara ya muziki nchi nzima.

Akizungumza Jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Operesheni wa TAMRISO Kelvin Msangi amesema wanahitaji mawakala watakaokusanya mapato kwenye biashara mbalimbali zinazopiga muziki katika mikoa zaidi ya 30 ya Tanzania Bara.

Aidha ameeleza kuwa mawakala hao wanatakiwa kuomba kibali ndani ya siku 30 kuanzia Leo huku akieleza utaratibu kuwa wanaotaka leseni hizo wanatakiwa kuingia kwenye mitandao ya Tamriso mawasiliano na fomu ya kujaza.

“Tunahimiza kampuni mbalimbali zinazotaka uwakala wa kukusanya mapato ya kazi za muziki kwenye majumba ya starehe, kwenye vyombo vya usafiri, mabasi, vyombo vya habari na sehemu zote zinazofanya biashara ya muziki wajitokeze tuweze kufanya nao kazi,” alisema.

Msangi amehimiza Jamii kutoa ushirikiano pindi mapato yatakapoanza kukusanywa na mawakala hao ili kuunga mkono juhudi za wasanii kwa kuthamini kazi zao lakini pia, juhudi za serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan za kuwania wasanii na kutaka kuona mafanikio kwao.

Pia, amewataka wasanii wote wa muziki kutoa ushirikiano hasa kwa kufuatilia vyombo vya habari vinavyopiga kazi zao ili waweze kupata fedha na kuongeza kuwa mwakani wasanii wataanza kulipwa mirabaha kulingana na mapato yatakavyokusanywa.

Tamriso walipewa jukumu la kutoa leseni hizo Julai mwaka huu baada ya kushinda zabuni iliyotangazwa na Ofisi ya Hakimiliki Tanzania (COSOTA) na sasa wanatarajia kuanza kazi rasmi.

Mwisho

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here
Captcha verification failed!
CAPTCHA user score failed. Please contact us!