
Na Boniface Gideon, Tanga
Chama cha National League for Democracy (NLD), kimeipongeza Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini kwa hatua stahiki ilizochukua hivi karibuni kwa baadhi ya vyama vya siasa kutokana na makada wa vyama hivyo kutoa kauli tata kwa jamii. Aidha, chama hicho kimewataka wanasiasa na vyama kuheshimu utaratibu na sheria za nchi na vyama vya siasa nchini.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Tanga Mei 24, Katibu Mkuu wa NLD, Doyo Hassan Doyo, amesema Msajili wa Vyama vya Siasa nchini ameonyesha ukomavu mkubwa baada ya kuchukua hatua za kisheria kwa vyama vya siasa ambavyo viongozi wake wanakwenda kinyume na sheria.
“Tumeona Msajili amewachukulia hatua Chadema kwa kuwaandikia barua ili wajieleze kutokana na makosa yao yanayowakabili, lakini pia tumeona Msajili amechukua hatua dhidi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili nao wajieleze kutokana na matamshi ya kada wao. Hii inaongeza matumaini makubwa kwa vyama vya siasa nchini na wananchi kwa ujumla,” ameongeza Doyo.
Doyo alivitaka vyama vya siasa nchini na wanasiasa kuheshimu taratibu na sheria za vyama vya siasa.
“Niwaombe wanasiasa nchini pamoja na vyama vya siasa kuheshimu taratibu na sheria za vyama vya siasa. Tukifuata taratibu tutaondoa mikanganyiko na sintofahamu ambazo huleta taharuki katika jamii,” amesisitiza Doyo.









