Mkuu wa Tawi la Utawala JKT Brigedia Jenerali Hassan Mabena, akizungumza na waandishi wa habari leo Mei 28,2026 katika Mako Makuu ya JKT Chamwino Mkoani Dodoma kuhusu wito wa vijana waliohitimu elimu ya sekondari kidato cha sita kwa mwaka 2026 kujiunga na mafunzo ya JKT.
Na.Alex Sonna-CHAMWINO
Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa JKT Meja Jenerali Rajab Mabele amewataka Vijana waliohitimu kidato cha Sita kwa Mwaka 2026 ambao wamechaguliwa kujiunga na Mafunzo ya JKT kwa Mujibu wa sheria kujiunga na mafunzo hayo katika makambi waliyochaguliwa kuanzia juni mosi, hadi juni 7, 2026.
Hayo yamesemwa leo Mei 28,2026 katika Mako Makuu ya JKT Chamwino Mkoani Dodoma kwa niaba ya Mkuu wa JKT, Mkuu wa Tawi la Utawala JKT Brigedia Jenerali Hassan Mabena amesema majina ya vijana wote waliohitimu kidato cha sita kwa Shule za Sekondari Tanzania Bara na Visiwani waliochaguliwa wanatakiwa kujiunga na mafunzo hayo.
Amesema orodha kamili ya majina ya vijana hao, makambi JKT waliyopangiwa, Maeneo ya Makambi hayo yalipo na vifaa wanavyotakiwa kwenda navyo inapatikana katika tovuti ya JKT ambayo ni www.jkt.mil.tz.
Amesema ilikufahamu kambi kijana aliyopangiwa atatakiwa kuingiza jina la shule au namba ya shule aliyohitimu kidato cha sita, mbele ya jina la shule ataona neno lililoandikwa waliochaguliwa ambapo akichagua neno hilo ataona majina ya waliochaguliwa kujiunga na mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria kwa mwaka 2026 na kambi aliyopangiwa.
Amesema ili kuona majina yote ya vijana na kambi walizopangiwa mtumiaji atapakua JKT PDF 2026 iliyopo juu kulia katika ukurasa huo.
Ameongeza kuwa Mkuu wa JKT Meja Jenerali Rajabu Mabele anawakaribisha vijana wote waliohitimu kidato cha sita kwa mwaka 2026 ili waweze kujiunga na vijana wenzao katika kujengewa uzalendo, kufundishwa nidhamu, ukakamavu, umoja wa kitaifa, stadi za kazi, stadi za maisha na utayari wa kulijenga na kulitumikia taifa.
Katika hatua nyingine amebainisha kuwa kwa wahitimu wenye ulemavu wa kuonekana kwa macho wataripoti katika kambi ya Ruvu JKT iliyopo Mlandizi Mkoani Pwani ambayo ina miondombinu ya kuwahudumia watu hao.











