Home Kitaifa MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA KUONGEZEKA MARA .

MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA KUONGEZEKA MARA .

Serikali ya Mkoa wa Mara kupitia Kaimu katibu tawala wa mkoa wa Mara ambaye pia ni Katibu Tawala Msaidizi Uchumi na Uzalishaji, Mhandisi Mwita Chacha Okayo leo Januari 30, 2026 imepokea mradi wa usambazaji na uuzaji wa majiko banifu kwa bei ya ruzuku.

Akizungumza wakati wa utoaji wa taarifa ya mradi, Mhandisi Mwandamizi kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Deusdedith Malulu amesema,

Kupitia tafiti iliyofanyika mwaka 2016 inakadiria kuwa takribani watu 33,024 hufariki kabla ya wakati kila mwaka kutokana na magonjwa ambayo yanachangiwa na uchafuzi wa hewa ndani ya nyumba wakati wa upikaji kwa kutumia nishati isiyo safi na salama ya kupikia na hii ni sawa na asilimia 8.49 ya vifo vyote nchini.

Hivyo, kwa kutambua hilo Serikali kupitia REA imekuja na mpango wa usambazaji na uuzaji wa majiko banifu kwa bei ya ruzuku ili kupunguza athari za kiafya na mazingira zitokanazo na matumizi ya nishati isiyo salama ya kupikia.

Halikadhalika, usambazaji na uuzaji wa majiko haya banifu ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa kitaifa wa matumizi ya nishati safi ya kupikia wenye dhima mpaka ifikapo mwaka 2034 zaidi ya asilimia themanini 80% ya watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia.

Aidha, katika kufanikisha hilo Wakala wa Nishati Vijijini unatarajia kusambaza na kuuza majiko banifu katika wilaya zote sita za mkoa wa Mara ambapo kwa wilaya za Butiama,Musoma, Serengeti na Rorya zitapata majiko 1,421 na wilaya za Tarime na Bunda zitapata majiko 1,420.

Aidha, mkataba wa mradi huu ulisainiwa kati ya REA na mtoa huduma Kampuni ya Geita Millenium Star Company Limited na utatekelezwa ndani ya miezi 15 ambapo mtoa huduma atasambaza na kuuza kwa bei ya ruzuku majiko banifu 8,486.

Aidha, gharama ya mradi ni zaidi ya TZS Milioni 297 ambapo serikali itatoa ruzuku ya asilimia themanini na tano (85%) sawa na zaidi ya TZS Milioni 252.4 hivyo badala ya jiko kuuzwa kwa bei ya awali ya TZS 35,000 litauzwa kwa bei ya ruzuku ya TZS 29,750 na mwananchi atachangia TZS 5,250 tu.

Aidha, Mhandisi Okayo ameipongeza REA kwa kuendelea kutekeleza kwa vitendo maono ya Mhe. Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha mwananchi anakuwa na uwezo wa kutumia na kupata nishati safi na salama ya kupikia yenye ufanisi mkubwa, rahisi na nafuu kupatikana.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here
Captcha verification failed!
CAPTCHA user score failed. Please contact us!