Na Boniface Gideon, MUHEZA
Baraza la Wanawake wa chama Cha Demokrasia na Maendeleo Chadema ( BAWACHA) Wilaya ya Muheza leo limefanya mafunzo maalumu ya kuwajengea uwezo wa kutambua fursa za Kiuchumi na matumizi sahihi ya fedha kwa Wanawake Wajasiriamali Wilayani humo.
Makamo Mwenyekiti wa chama hicho Kanda ya Kaskazini Yosepha Komba aliwaambia Waandishi wa Habari kuwa lengo la mafunzo hayo nikuwajengea uwezo Kiuchumi Wanawake nakuwafanya kuwa imara Kiuchumi na kupunguza utegemezi katika Jamii,
“Kama tunavyofahamu Chama chetu kinawategemea Sana Akinamama na Chama Kinawathamini Akinamama hivyo kwakuona hilo tumeona kuwapatie Mafunzo maalumu ya Ujasiriamali ili wainuke Kiuchumi lakini pia wakienda huko wakatoe Elimu hii kwa wengine” Alisema Yosepha
Yosepha Alisema lengo ni kuwafikia Wanawake zaidi ya 5,000 hivyo mafunzo hayo ni endelevu,
“Tunaendelea kutoa mafunzo haya na Leo tumeanza na Wanawake zaidi ya 50 na tumeona changamoto zao kubwa ni mitaji soko la Biashara husika lakini Wengi wao wanaenda kukopa kwenye mikopo kausha Damu ambayo huwafanya wadidimie zaidi hivyo tumewapatia Elimu sahihi ya namna ya kupata mitaji na kutambua soko la Biashara” Alisema Yosepha
Kwa upande wake Mkufunzi wa mafunzo hayo George Chambai Alisema changamoto kubwa zinazowakumba Wanawake Wajasiriamali nikuchukua mikopo Umiza ambayo inawafanya kurudi nyuma Kiuchumi.
“Mikopo Umiza ni hatari sana na hii imewafanya Wanawake wengi kurudi nyuma Kiuchumi na kudharirika kwakuwa wanawachukulia mpaka vitu vya ndani” alisema Chambai
Aliwataka Wanawake kuwekeza fedha kidogo kidogo ili wapate fedha za akiba ,
“Sisi wataalamu wa uchumi tunawashauri watumie njia m’badala kupata mitaji ikiwemo kuwekeza kidogo kidogo na kama wanataka mikopo waende kwenye Taasisi za kifedha kama Benki na wapatiwe Elimu kabla ya kuchukua mkopo” Alisisitiza Chambai
Mwisho








