
Na Boniface Gideon, TANGA
Wadau wa sekta ya nishati wanaendelea kusisitiza umuhimu wa matumizi ya nishati safi ili kulinda afya za wananchi na mazingira, huku jitihada za uhamasishaji zikiendelea kuimarika nchini.
Kampuni ya Taifa Gesi imesema ni miongoni mwa washiriki katika juhudi hizo, ikieleza kuwa imewekeza katika miundombinu ya kuhifadhi na kusambaza gesi ili kuongeza upatikanaji wake kwa wananchi.
Meneja wa Masoko wa kampuni hiyo, Oscar Shelukindo, amesema matumizi ya gesi yanaweza kusaidia kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, ambavyo vimekuwa vikihusishwa na athari za kiafya na kimazingira.
Kwa mujibu wa takwimu, matumizi ya nishati zisizo safi yanachangia vifo vya zaidi ya Watanzania 33,000 kila mwaka, hali inayoonyesha umuhimu wa kuhamia katika nishati mbadala.
Katika kuendeleza uhamasishaji huo, wadau mbalimbali wanaendelea kutoa elimu kwa umma kupitia majukwaa tofauti, wakilenga kuongeza uelewa na matumizi ya nishati safi nchini.








