Na Boniface Gideon, TANGA
MAMLAKA ya maji Safi na usafi wa Mazingira Tanga (Tanga uwasa) jana imekabidhi vyoo kwa shule za msingi na sekondari Funguni hii ikiwa ni sehemu ya mradi mkubwa wanaoutekeleza wilayani Pangani wa kutibu taka ngumu uliogawanywa katika sehemu kuu tatu za ujenzi wa miundombinu ya kupokea na kutibu taka ngumu uliopo mbioni kukamilika ukifikia 92%, ujenzi wa vyoo katika maeneo matatu ya shule ya msingi na sekondari Funguni iliyokwisha kukamilika kwa 100% pamoja na eneo la kituo kikuu cha mabasi uliofikia 98% hii ikilenga hasa kuwakinga na magonjwa ya mlipuko wananchi wanaozunguka maeneo hayo.
Miradi hiyo inayotekelezwa na Mkandarasi M/S PERNTELS COMPANY. Ltd kwa gharama ya shilingi Billion moja ambazo ni ufadhili wa serikali na inatarajiwa kukamilika na kukabidhiwa Septemba, 2023.
Akitoa taarifa ya utekelezaji wa miradi hiyo mkurugenzi mtendaji wa mamlaka ya maji Safi na usafi wa Mazingira (Tanga Uwasa) Mhandisi Geofrey Hilly amesema kuwa miradi hiyo inatekelezwa kupitia ufadhili wa serikali ambapo kupitia mbunge wa Jimbo la Pangani na waziri wa maji Jumaa Aweso kiasi cha shilingi Billion moja kilitolewa kwaajili ya kutekeleza mradi huo.
“Katika mradi huu tumelenga kwaajili ya kutoa maji ambayo baada ya kuyatibu yawe ni maji safi na salama Tanga Uwasa imetekeleza mradi huu kwa lengo la kuboresha huduma kwa wakazi wa mji wa Pangani na nje ya Pangani kwa ujumla na mradi huu umejengwa kwa ufadhili wa serikali kwa gharama ya shilingi billion moja utekelezaji na gharama baada ya kupata bajeti na kufanya mchakato wa ununuzi mradi ilipatikana kwa shilingi million 998 na lengo la mradi kwa ujumla wake ni kukamilika September 30,2023.” alisema Mhandishi Hilly.
“Kazi zilizotegemewa na ambazo zimefanyika kulikuwa na ujenzi wa mtambo wa kuchuja maji taka ambao umefikia 92%, kujenga vyoo vitatu eneo la shule ya msingi na sekondari Funguni na kituo cha mabasi, pia kulikuwa na utaratibu wa kupata gari la kunyonya maji taka na tayari lipo tayari litakuja kwaajili ya makabidhiano lakini pia tulihakikisha kuwa waliotupa maeneo ya mradi wamepata stahiki zao” aliongeza .
Akikabidhi moja ya mradi wa choo katika shule ya msingi Funguni tayari kwa kuanza kutumika mkuu wa wilaya ya Pangani Zainab Abdallah aliwapongeza Tanga Uwasa kwa kuendelea kufanya huduma zake na kuwafikia wananchi karibu sambamba na kujali afya zao kwa kujenga vyoo katika maeneo yanayowazunguka.
“Kwa niaba ya serikali tunawashukuru sana Tanga Uwasa kwa kazi kubwa wanayofanya katika kuhudumia wananchi wa Pangani , tunaona mradi huu wa kuhakikisha maji taka yanaweza kudhibitiwa nimpongeze sana mbunge kwa kuhakikisha fedha hizi zinapatikana lakini pia wamefikia jamii kwa kujenga vyoo katika shule yetu ya msingi na sekondari Funguni lakini na stendi tunawapongeza sana” alisema Zainab.
Kwa upande wake mwenyekiti wa chama cha mapinduzi ‘CCM’ wilaya ya Pangani Abdallah akiwa katika ziara ya kamati ya siasa kukagua miradi ya maendeleo pamoja na kuongea na wananchi amewapongeza Tanga Uwasa kwa kutekeleza miradi hiyo.

Mwisho








