Home Kitaifa SERIKALI INACHUKUA HATUA KUKABILI UPANDAJI WA BEI ZA BIDHAA MUHIMU

SERIKALI INACHUKUA HATUA KUKABILI UPANDAJI WA BEI ZA BIDHAA MUHIMU

Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Dkt Ashatu Kijaji aeleza hatua zinazochukuliwa na Serikali ili kuwapunguzia Wananchi athari zitokanazo na kupanda kwa bei ya bidhaa muhimu.

Kauli hiyo ameitoa jana Agosti 15, 2022 Jijini Dodoma wakati alipokuwa akiongea na waandishi wa Habari juu ya tathmini ya mwenendo wa Bei ya Bidhaa muhimu Nchini ambapo Wizara inashirikiana na Tume ya Ushindani (FCC) na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kutekeleza jukumu la kufuatilia na kufanya tathmini ya mwenendo wa bei za bidhaa muhimu nchini.

Dkt. Kijaji amesema kuwa hatua hizo ni pamoja na kuwapunguzia gharama za uzalishaji, uagizaji na usambazaji wa bidhaa ili kuleta uhimilivu wa bei kwenye soko lengo likiwa ni kumlinda mlaji kwa kuhakikisha anapata bidhaa bora kwa bei stahiki na kuzuia upandishwaji holela wa bei ya bidhaa mbalimbali.

Matokeo ya tathmini zilizofanyika hivi karibuni yalionesha kuwa kuna uhimilivu mkubwa wa bei kwa bidhaa zinazozalishwa hapa nchini, ambazo zilionesha ongezeko dogo la bei ikilinganishwa na bidhaa zinazoagizwa kutoka nje ya nchi ambazo zilionesha ongezeko kubwa zaidi la bei. ” Amesema Dkt Kijaji.

Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, imefanya jitihada kubwa za kuweka mazingira rafiki ya ufanyaji biashara nchini, kwa kuchukua hatua mbalimbali katika kudhibiti ongezeko la bei ya bidhaa ikiwa ni pamoja na udhibiti wa upandishwaji holela wa bei za ndani na soko la Dunia “ Ameongeza.

Niwataarifu kuwa Serikali kupitia Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka wa fedha 2022/2023 na Sheria ya Fedha ya mwaka 2022 hatua tuliyoichukua kuondoa kodi ya ongezeko la thamani kwa wazalishaji wa ndani mafuta ya kupikia yaliyosafishwa ikiwa pia tunaendelea kuhamasisha uzalishaji wa mbegu za mafuta ya kupikia nchini hasa alizeti na chikichi” Amesema Dkt.Kijaji.

Pia amesema Serikali imeondoa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwa wazalishaji wa mbolea kwa kipindi cha mwaka mmoja ili kuwapunguzia wakulima gharama za uzalishaji na hivyo kuleta unafuu wa bei ya mazao muhimu ya chakula pamoja na kupunguza ushuru kwa maroli yanayosafirisha bidhaa.

Amesema katika sekta ya zao la Ngano Serikali inatekeleza Mkakati wa kuongeza uzalishaji wa zao hilo nchini ili kukabiliana na upungufu wa tani 800,000 wanazoagiza kila mwaka huku kiasi kikubwa kikitoka katika nchi za Urusi na Ukraine.

Wizara yetu ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara inaunga mkono jitihada za Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan za kuifungua nchi, kuvutia uwekezaji na utalii kwa kutafuta masoko ya bidhaa zinazozalishwa nchini na tayari tumepata matokeo ambapo kwa mwezi Agosti, 2022, fursa mbalimbali zimepatikana katika masoko ya Kimataifa .

Vifaa vya Ujenzi na Saruji kuwa Kwa sasa nchi ina jumla ya Viwanda 17 vya Saruji vyenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya saruji hapa nchini na kwamba Wastani wa bei ya nondo za 10mm ilikuwa kati ya Shilingi 19,000 na 23,000 kwa mwezi Julai na Shilingi 18,000 hadi 23,000 kwa mwezi Agosti; 2022.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here
Captcha verification failed!
CAPTCHA user score failed. Please contact us!