
Na Shomari Binda-Musoma
MKUU wa mkoa wa Mara Kanali Evans Mtambi ameagiza kusakwa na kukamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria wezi wa taa za barabarani.
Kauli hiyo ameitoa leo machi 4, 2025 kwenye kikao cha bodi ya baraɓara mkoa wa Mara kilichofanyika kwenye ukumbi wa uwekezaji.
Akizungumza mara baada ya kutolewa kwa taarifa ya Wakala wa Barabara ( TANROADS) mkoa wa Mara amesema haikubariki kuona wizi huo unaendelea kwa maslahi ya watu binafsi wasiopenda maendeleo.
Amesema serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali za maendeleo lakini wapo wachache wanaotaka kukwamisha ambao hawawezi kuvumiliwa.
Mtambi amesema wizi ulioripotiwa hauwezi kuvumilika na kuagiza jeshi la polisi kuwasaka wezi hao na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

” Naagiza kusakwa kwa wezi hawa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria ili hatua ziweze kuchukuliwa dhidi yao maana huu ni uhujumu uchumi.
” Taa hizi zinawasaidia wananchi hata kwenye shughuli zao za uchumi lakini watu wachache kwa maslahi binafsi wanataka kuturudisha nyuma lazima tushughulike nao”,amesema.
Awali akiwasilisha taarifa yake meneja wa TANROADS mkoa wa Mara mhandisi Vedastus Maribe ameitaja Wilaya ya Bunda kuwa vinara wa wizi wa taa za barabarani.
Maribe ameviomba vyombo vya dola kuhakikisha wanawafatilia wezi hao kwa kuwa wanakwamisha juhudi za serikali kuwaletea wananchi maendeleo.
Akichangia kwenye kikao hicho mbunge wa jimbo la Tarime vijijini Mwita Waitara ameomba taa zilizopo Bunda zihamishiweTarime vijijini kwa kuwa kunakofanyika wizi wa taa hawataki maendeleo.









