
Na. Saidina Msangi, WF, Abidjan, Côte d’Ivoire.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mshamu Ali Munde, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, ameongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire kuanzia tarehe 23 hadi 24 Julai, 2026.

Mkutano huo utawakutanisha Mawaziri wa Fedha, Madini, Biashara, Viwanda, Mipango ya Uchumi, Magavana wa Benki Kuu pamoja na viongozi wa taasisi mbalimbali za Umoja wa Afrika na mashirika ya kifedha ya kikanda kujadili mikakati ya kuharakisha maendeleo ya viwanda barani Afrika kupitia upatikanaji wa rasilimali fedha, biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi.
Miongoni mwa masuala ya sekta ya fedha yatakayojadiliwa ni namna ya kuongeza wigo wa fedha za maendeleo ya viwanda, usimamizi wa deni la umma, ukusanyaji wa mapato, kuimarisha masoko ya mitaji na ushiriki wa sekta binafsi katika maendeleo ya viwanda, kuendeleza mageuzi ya mfumo wa fedha wa kimataifa ili kuziwezesha nchi za Afrika kupata rasilimali kwa masharti nafuu.

Aidha, mkutano huo utajadili athari za migogoro ya kimataifa kwa uchumi wa Afrika, hali ya maendeleo ya viwanda barani Afrika, ujenzi wa shoroba za kimkakati zinazoweza kuchochea ukuaji wa uchumi, maendeleo ya viwanda pamoja na hatua za kuimarisha biashara ya ndani ya Afrika kupitia utekelezaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA).
Ushiriki wa Tanzania katika mkutano huo unatoa fursa ya kuwasilisha uzoefu wa nchi katika usimamizi wa uchumi, ukusanyaji wa rasilimali za ndani kwa ajili ya maendeleo, pamoja na juhudi zinazoendelea za kuboresha mazingira ya uwekezaji na kuharakisha maendeleo ya viwanda kwa ushirikiano na sekta binafsi, sambamba na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano.
Pia ushiriki wa Tanzania kwenye Mkutano huo, wenye kaulimbiu “Kufadhili Maendeleo ya Viwanda barabi Afrika kwa Maendeleo Endelevu’’, unaonesha dhamira ya Serikali ya kuendelea kushirikiana na nchi nyingine za Afrika katika kutafuta suluhu kuhusu za changamoto za maendeleo na kuweka mazingira bora ya kukuza viwanda, biashara na uwekezaji.
MWISHO.









